
Mshambuliaji wa
zamani wa klabu ya Chelsea na Celtic Chris Sutton ameendelea
kumkandia kocha wa klabu ya Arsenal kwa kusema kwamba kamwe Klabu hiyo isitarajie
ubingwa kama timu hiyo itaendelea kuwa chini ya ya mkufunzi huyo. Katika
dirisha hili la usajili Arsenal wamemsajili Granit Xhaka tu, huku wenzao
Manchester City, Manchester United na Chelsea wakiwa wamefanya usajili wa maana
kuimarisha vikosi vyao kwaajili ya msimu mpya.
Sutton ambaye alibeba kombe la Ligi ya England akiwa na
Blackburn Rovers, amemlaumu Arsene Wenger kwa kutoonesha nia ya dhati ya
kufanya usajili wa kusiaidia timu na kusisitiza Mfaransa huyo anahitaji kuachia
ngazi kwa manufaa ya timu.
“Nina mashaka makubwa na Arsenal katika msimu huu tena.
Hawajaonesha nia yoyote mpaka sasa,”Sutton aliiambia BBC Five.
“Nadhani bodi na Wenger wanawaangusha sana mashabiki wao.
Mimi sijui ni wapi Arsenal wanaelekea, kama ningekuwa ni shabiki wa Arsenal,
basi ningehuzunika sana.
“Wamesema hawatatumia fedha nyingi, bodi inafurahia tu
jambo hili, au uongo? Kila mwaka, wao kazi yao ni kushiriki Ligi ya Mabingwa na
kupata fedha.
“Wenger sio kocha mwenye malengo na Arsenal tena, alikuwa
na nafasi kubwa ya kushinda taji msimu uliopita, lakini alishindwa. Hawataki
kutumia pesa, na kama wewe ni shabiki wa Arsenal, jitathmini vizuri, maana kila
mwaka itakuwa ni mwendo wa ‘top four’ tu.
Halafu unaona timu kama Manchester United, Manchester
City wanaonesha nia ya ubingwa msimu huu, hili linazidi kuleta ugumu zaidi kwa
Arsenal, nasema hivi….mpaka Wenger aondoke ndipo Arsenal watatwaa ubingwa.”
Hayo ni maneno ya Sutton akionyesha waziwazi kumkandia kocha Arsene Wenger kwa kusema kwamba, kuendelea
kuwepo kwake klabuni hapo, ndiyo sababu ya klabu hiyo kutokutwaa mataji. Kumbe
Sutton anamaanisha mafanikio ya klabu hiyo ni siku wamemwacha mkufunzi huyo
raia wa Ufaransa na kumsajili kocha mwingine, ndiyo watapata mafanikio.
Post a Comment