
BAADA ya mapumziko
ya takribani ya wiki tatu kupisha michuano mbalimbali ya kimataifa kwa ngazi ya
timu ya taifa na klabu, kadhalika michuano ya Kombe la Azam Sports Federation
Cup, Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara (VPL) inarejea tena leo Jumamosi April
1, 2017 kwa michezo miwili.
Mechi ya kwanza
itawakutanisha mabingwa watetezi wa ligi hiyo, timu ya Yanga watakaokuwa
wakichuana vikali na matajiri wa jiji la DSM, timu ya Azam FC kwenye dimba la
taifa majira ya saa kumi za jioni.
Kadhalika,
katika uwanja wa kumbukumbu ya Sokoine jijini Mbeya, Mbeya city watakuwa
wenyeji wa Ruvu shooting yenye makazi yao Mlandizi mjini Pwani.
Mechi za ligi hiyo ambazo huoneshwa mubashara
na Kituo cha Televisheni cha Azam ambacho ni mdhamini mwenza wa VPL, itaendelea
kesho Jumapili April 2, 2017 ambako Kagera Sugar inatarajiwa kuwa mwenyeji wa
Simba kwenye Uwanja wa Kaitaba, Bukoba mkoani Kagera. Mchezo huo utakuwa saa
10:00 jioni.
Mchezo mwingine utazikutanisha timu za African
Lyon ya Dar es Salaam dhidi Stand United ya Shinyanga utakaofanyika Uwanja wa
Uhuru, Dar es Salaam. Mchezo huu, utaanza saa 8:00 mchana kwa kuwa kanuni
zinaridhia.
Mtibwa Sugar ya Morogoro watakuwa wageni wa
Tanzania Prisons ya Mbeya kwenye Uwanja wa Sokoine jijini humo wakati Mwadui
FC, kwa upende wake watawaalika JKT Ruvu ya Pwani kwenye Uwanja wa Mwadui huko
Shinyanga huku Majimaji wakiwa ni wenyeji wa Toto Africans kwenye Uwanja wa
Majimaji mjini Songea.
Post a Comment