
RAUNDI ya tano ya
mashindano ya FA [Azam Sports Federatio Cup] imeendelea leo uwanja wa Uhuru
jijini Dar es salaam ambapo Ashanti United walikuwa na kibarua kizito cha
kuwakabili mabingwa watetezi wa kombe hilo, timu ya Yanga.
Licha ya kucheza mpira
wa wazi bado haikuwa rahisi kwa Ashanti United ambao mpaka filimbi ya mwamuzi
inapulizwa kuashiria mwisho wa mchezo, Yanga walikuwa na 4 wakati Ashanti
wakipachika bao 1 pekee.
Goli la kwanza la
Yanga lilifungwa na mshambuliaji wa timu hiyo Amis Tambwe ambaye
aliunganisha pasi iliyopigwa toka upande wa kulia na Msuva.
Dakika 37 Yanga
walipata bao la pili kupitia kwa Thaban Kamusoko baada kuachia shuti kali
nje ya kumi na nane lilomshinda mlinga lango wa Ashanti, Rajabu Kahumbu.
Msuva alifunga bao la
tatu dakika ya 53 kwa penati baada ya Seleman Sultan kumchezea vibaya Msuva na
muamuzi Ahmad Kikumbo kuamuru penati ipigwe na winga huyo akaweka mpira
kambani.
Goli pekee la Ashanti
lilifungwa dakika 61 na Isack Hassan ambaye aliwazidi ujanja mabeki wa Yanga.
Yusuph Muhilu
alikamilisha karamu ya magoli dakika ya 89 baada ya kufunga bao la nne kwa
kumalizia krosi ya Emmanuel Martin toka upande wa kushoto.
Kesho kutakuwa na
mchezo mwingine katika michuano hii kati ya Simba na Polisi Dar katika uwanja
wa Uhuru jijini Dar es Salaam.
Post a Comment